![]() |
PROFILE PHOTO: 'Nay wa Mitego' |
DODOMA.
Waziri wa Habari, utamaduni, sanaa
na michezo, Dkt Harrison Mwakyembe ameliomba jeshi la polisi kumuachia msanii
wa Bongofleva Emmanuel Elibariki maarufu kama “Nay wa Mitego” aliyekuwa
anashikiliwa kwa tuhuma za kutoa wimbo usio na maadili uliojulikana kama
“WAPO”.
Akizungumza mjini Dodoma, Mwakyembe amesema kuwa
aliwasiliana na Rais ambaye alimuelekeza kuwa wimbo huo haukuwa na shida yoyote
ya kimaadili na kwamba hata yeye binafsi ameupenda na anamtaka msanii huyo
aongeze baadhi ya mabeti kwenye wimbo wake.
“Kwakweli
ule wimbo ni mzuri hata mheshimiwa Rais amesema anaupenda na kusema ukweli ile
biti imetulia,” amesema waziri Mwakyembe wakati akitoa ufafanuzi kuhusiana
na wimbo huo.
Waziri Mwakyembe amesema kuwa Rais Magufuli amependekeza
kwenye wimbo wake aongeze kama maneno “hata wakwepa kodi...wapoo”! Ili kuufanya
unoge zaidi kutokana na ujumbe wake kuwa ulilenga kuiamsha jamii juu ya athari
za utawala mbaya na rushwa kwenye jamii.
“Nimechukua
hatua kama waziri mwenye dhamana kuwaomba polisi kumuachia huyo kijana,
wamuache kumuhoji na hata nitafurahi nikimuona kesho akija Dodoma ili nimshauri
nini cha kufanya kwenye wimbo wake ili uwe mzuri zaidi,” alisema
waziri Mwakyembe.
Waziri Mwakyembe ameongeza kuwa wao kama Serikali na wizara
hawaoni madhara ya wimbo huo lakini akataka uboreshwe zaidi na kuwataja watu
kama wakwepa kodi na wanaojihusisha na dawa za kulevya.
Post a Comment