0
Vyuo Vikuu hapa Nchini vimeagizwa kuacha mara moja kutoza ada kwa fedha za kigeni kwa wanafunzi ambao ni watanzania, vinginevyo hatua kali za kisheria zitatumika kwa yeyote atakayepatikana akitoza ada kwa fedha hizo.

Naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia mhandisi Stella Manyanya.

KUTOKA DODOMA.
Agizo hilo limetolewa jana Bungeni mjini Dodoma na naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia mhandisi Stella Manyanya alipokuwa akijibu swali lililoulizwa na Mbunge Jaku Hashimu Ayoub kuwa kumekuwa na malalamiko ya wanafunzi wa Elimu ya Juu Tanzania ambao ni wazawa kulipishwa ada ya masomo kwa fedha za kigeni badala ya fedha za Kitanzania.

“Sarafu inayotakiwa kutumika Tanzania ni shilingi ya Kitanzania kwa mujibu wa kifungu cha 25 na 26 cha Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania (BOT) ya mwaka 2006. Aidha, kwa Tanzania malipo ya kitu au huduma yoyote inapaswa kulipwa kwa shilingi ya Kitanzania kama ilivyoainishwa kwenye kifungu cha 28 cha Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania 2006” alifafanua Mhandisi Manyanya.

Aliendelea kwa kusema kuwa mpaka sasa wizara haijapokea malalamiko yoyote ya kutozwa fedha za kigeni kwa wanafunzi wa elimu ya juu tangu itoe agizo kama hilo kwa wamiliki wa vyuo Septemba 07, 2016.

Ikiwa ni kwa mara nyingine Mhandisi Manyanya ameviagiza vyuo ambavyo bado vinatoza wanafunzi Watanzania fedha za kigeni kuacha mara moja kwani vyuo hivyo vimeelekezwa kutoza wananchi wa Kitanzania kwa pesa ya Kitanzania.

Aidha Mhandisi Manyanya  amewataka watanzania kutoa taarifa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ikiwa kuna Chuo chochote kinachotoza ada kwa Watanzania kwa fedha za Kigeni ili hatua stahiki za kisheria zichukuliwe dhidi ya wahusika.

Waziri wa fedha na mipango Philip Mpango.

Wakati huohuo Waziri wa Fedha na Mipango Philip Mpango alitoa onyo kwa shule zinazotoza ada kwa fedha za kigeni kuchukuliwa hatua kali za kisheria ambapo alisema, ikiwa kuna mwananchi yeyote anayetozwa ada kwa fedha za kigeni basi atoe taarifa mapema ili hatua stahiki zichukuliwe kwa wahusika..

Post a Comment

 
Top